Klabu ya Simba SC imeshindwa kukamilisha usajili wa mshambuliaji Paul Peter Kasunda kutoka JKT Tanzania, baada ya muda wa kukamilisha uhamisho huo kuisha.
Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana, JKT Tanzania ilikuwa imeitaka Simba kukamilisha usajili wa mshambuliaji huyo kabla ya saa 12 jioni, ili kutoa nafasi kwa klabu hiyo ya kijeshi kupata muda wa kutafuta na kumsajili mbadala wake.
Hata hivyo, taarifa zinaeleza kuwa Simba iliwasiliana na JKT Tanzania majira ya saa 4 usiku, wakati ambapo muda wa usajili ulikuwa umekwisha na maafande hao tayari walikuwa wameamua kusitisha uhamisho huo kutokana na ufinyu wa muda wa kupata mbadala wa Kasunda.
Inaelezwa pia kuwa kulikuwa na mvutano ndani ya uongozi wa Simba kuhusu usajili wa mshambuliaji huyo, huku baadhi ya viongozi wakipinga hatua hiyo, hasa baada ya klabu hiyo kumsajili Ismail Mgunda.
Katika hatua nyingine, kulikuwa na mapendekezo ndani ya Simba ya kusajili mshambuliaji wa kigeni au kiungo mkabaji, lakini mipango hiyo nayo haikuweza kutekelezwa.
Kwa sasa, Simba imefunga dirisha lake la usajili kwa kuwaongeza kikosini Ismail Mgunda pamoja na beki Ibrahim Nindi. Aidha, mpango wa kumsajili kiungo Feisal Salum ‘Fei Toto’ pia haukufanikiwa.