Mshambuliaji wa Yanga, Cheikh Ibrahima Toure, ameweka wazi kuwa hana presha kutokana na kutofunga mabao mengi tangu alipojiunga na klabu hiyo, akiamini kuwa muda wake wa kuonyesha uwezo mkubwa na kuwafurahisha mashabiki wa Yanga bado unakuja.
Toure, ambaye alisajiliwa na Yanga msimu huu akitokea Saudi Arabia, hadi sasa amefanikiwa kufunga bao moja katika mechi tano za Ligi Kuu Bara. Hata hivyo, idadi hiyo haijamfanya mshambuliaji huyo kuingiwa na hofu kuhusu kiwango chake.
"Sina sababu ya kuwa na presha, kwani naamini kadiri ninavyozoea mazingira ya soka la Tanzania na mfumo wa Yanga, ndivyo nafasi yangu ya kufunga mabao mengi itakavyoongezeka," alisema
Mbali na kuzungumzia kiwango chake, Touré ameeleza kuvutiwa na ushindani uliopo katika Ligi Kuu Tanzania.
Mshambuliaji huyo amesema ligi imemvutia kutokana na ushindani wake mkubwa, hasa upande wa nguvu za mwili, akieleza kuwa imekuwa tofauti na baadhi ya matarajio aliyokuwa nayo kabla ya kuwasili nchini.
Akizungumzia mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Gaborone United utakaopigwa uwanja wa Azam Complex hapo kesho, Toure amesema wamekuwa na maandalizi mazuri kuelekea mchezo huo na matarajio yake ni Yanga kuibuka na ushindi na kutinga raundi ya kwanza.