Beki Ibrahim Hamad ‘Bacca’ ameendelea kujidhihirisha kama mmoja wa nguzo muhimu katika safu ya ulinzi ya Yanga SC, baada ya beki huyo wa kati kucheza mechi zote saba za mashindano ambayo timu hiyo imekabiliana nayo msimu huu, akitumika kwa dakika zote 630.
Bacca ameanza msimu akiwa sehemu ya kikosi cha kwanza chini ya Kocha Mkuu Manqoba Mngqithi, na kuendelea kwake kupewa nafasi katika kila mchezo kunaonyesha wazi umuhimu wake katika mipango ya kocha huyo.
Katika safu ya ulinzi, jukumu la Bacca halihusiani tu na kuzuia mashambulizi ya wapinzani. Beki huyo pia anasaidia timu kuwa na utulivu inapokuwa chini ya presha na kuchangia ujenzi wa mashambulizi kuanzia eneo la nyuma.
Miongoni mwa viashiria vikubwa vya kuaminiwa kwake ni ukweli kwamba hajapitwa na mchezo hata mmoja tangu msimu ulipoanza. Katika mechi tano za Ligi Kuu Bara ambazo Yanga imecheza hadi sasa, Bacca ameanza zote, huku pia akiwa sehemu ya kikosi kilichocheza Ngao ya Jamii na mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Kwa lugha rahisi, Mngqithi amempa Bacca jukumu la kuwa sehemu ya msingi ya ukuta wa Yanga akionekana kumuamini mepema tu.
Katika dirisha lililopita, Yanga ilimsajili Oumar Farouk Komara kuongeza nguvu katika eneo hilo, huku Dickson Job akitarajiwa kurejea baada ya kupona jeraha.
Komara tayari amepewa nafasi ya kucheza mchezo wa ligi kuu dhidi ya Fountain Gate akichukua nafasi ya nahodha Bakari Mwamnyeto huku kurejea kwa Job kukimaanisha kwamba Mngqithi sasa ana machaguo zaidi katika safu ya nyuma.
Dakika 630 zinasema kila kitu
Bacca amekusanya dakika 630 ndani ya mechi saba, jambo linalomweka miongoni mwa wachezaji ambao wamepewa majukumu makubwa zaidi na benchi la ufundi la Yanga mwanzoni mwa msimu huu.Yeye na mlinda lango Djigui Diarra wamecheza dakika zote za mechi kila ya mechi ya kimashindano.
Kwa beki wa kati, kucheza kila dakika katika michezo hiyo kunaonyesha zaidi ya uimara wa mwili. Kunaonyesha pia kiwango cha imani ambacho kocha anakuwa nacho kwa mchezaji wake.
Bacca ameimarika sana katika ujenzi wa mashambulizi kutokea nyuma, kushinda mipambano ya mipira na kuhakikisha safu ya ulinzi haivurugiki, hasa wakati Yanga inapokutana na wapinzani wanaobadilisha kasi ya mchezo.
Si Ulinzi Pekee
Ingawa jukumu lake kubwa ni kulinda lango la Yanga, Bacca pia ameonyesha uwezo wa kuchangia katika eneo la ushambuliaji.
Msimu huu tayari amefunga bao moja dhidi ya JKT Tanzania, akiongeza kwenye rekodi yake ya kufunga bao moja aliyokuwa nayo msimu uliopita.
Hata hivyo, thamani yake kubwa kwa Yanga haipimwi kwa mabao, umuhimu wake unatokana zaidi na namna anavyosaidia timu kupata utulivu nyuma, kuanza mashambulizi kutoka eneo la ulinzi na kudumisha uwiano wa timu inapokuwa na mpira.