Baada ya kufanyiwa tathmini ya kitabibu kubaini uponaji wa majeraha yaliyokuwa yanawakabili, wachezaji Clement Mzize na Dickson Job sasa wako tayari kurejea uwanjani kuendelea na majukumu yao.
Nyota hao walisafiri na kikosi cha Yanga wakati kinaelekea Botswana ambapo wao waliishia Afrika Kusini kwa ajili ya kufanyiwa vipimo.

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe amethibitisha kuwa wachezaji hao sasa wameruhusiwa kurejea uwanjani baada ya kuonekana sasa hawana tatizo.
“Habari njema kutoka kwa wataalamu wetu wa masuala ya kitabibu wanasema kuwa wachezaji wetu Dickson Job na Clement Mzize, ambao walisafiri kwenda Afrika Kusini kwa ajili ya vipimo, wapo salama na wanajiandaa kurejea uwanjani."
"Kimsingi, wachezaji hawa wawili ni kama usajili mpya kwetu, Wale ambao mmecheza na Yanga na hamkukutana na Clement Mzize Bull Striker basi Niwaambie tu kwamba Mzize na Job wamerudi,” alisema Kamwe
Mzize amekosekana kwa takribani msimu mzima wakati Job aliumia mwezi Machi mwaka huu kwenye mchezo wa ligi kuu dhidi ya Simba uliopigwa uwanja wa New Amaan Complex.
Unaweza kusema sasa ni suala la muda wawili hao wataonekana kwenye kikosi cha kocha Manqoba Mngqithi.