Baada ya mapumziko ya siku moja kikosi cha Yanga leo kinatarajiwa kuendelea na maandalizi ya mchezo wa mkondo wa pili hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Gaborone United.
Mchezo huo utapigwa Jumamosi, Septemba 12 katika uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es salaam.
Akizungumza jana muda mfupi baada ya kikosi chak kurejea kutoka Botswana, Kocha Mkuu wa Yanga Manqoba mngqithi alisema sare ya bao 1-1 ugenini sio matokeo mabaya lakini anataka kuona vijana wake wakimaliza mchezo hapa nyumbani.
Licha ya kikosi chake kutawala mchezo, Manqoba alieleza kutorodhishwa na baadhi ya maeneo akiahidi kufanyia kazi kwenye uwanja wa mazoezi.
“Hatupo sehemu mbaya sana, ukitazama tunatengeneza nafasi lakini tunatakiwa kuongeza njaa ya kuzitumia, nakubali kwamba tunapoteza naadhi ya nafasi lakini bado tunatakiwa kuwa bora kwenye kutengeneza nafasi zaidi ya tunachofanya sasa"
“Ukiangalia kuna changamoto bado kwenye utengenezwaji wa mashambulizi ya pembeni, bado krosi nyingi zinakuwa sio muafaka sana na zingine zinapotea, hili linatakiwa kurekebishwa tunaendelea kulifanyia kazi.
“Ukiacha pembeni, tumeanza kutengeneza nafasi kutoka katikati ya uwanja lakini bado tunatakiwa kuongeza ubora zaidi, bahati mbaya kuna wachezaji bado tunawajenga ambao wanaweza kutupa kitu zaidi eneo hilo,” alisema Manqoba
Kwenye mchezo wa marudiano Yanga itahitaji ushindi ili kujihakikishia kutinga raundi ya kwanza.