Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Klabu ya Yanga, Ally Kamwe, ametangaza rasmi kuwa Jumamosi hii itakuwa 'Sele Day', kuelekea mchezo wa marudiano wa Ligi ya Mabingwa barani Afrika dhidi ya Gaborone United kutoka Botswana.
Mchezo huo wa hatua ya awali unatarajiwa kupigwa Septemba 12, katika Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 usiku.
Akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kikosi cha Yanga kurejea Dar wakitokea Botswana, Kamwe amesema uongozi umeamua kuifanya siku hiyo kuwa maalum kwa ajili ya mshambuliaji wao, Seleman Mwalimu 'Gomez', ambaye alifunga goli muhimu la kusawazisha na kuinusuru timu hiyo katika mchezo wa kwanza uliomalizika kwa sare ya 1-1 ugenini nchini Botswana.
"Jumamosi tunakwenda Azam Complex, na tumetangaza rasmi kuwa hiyo itakuwa 'Sele Day'. Ili kunogesha ushangiliaji na kuonyesha sapoti kwa Seleman Mwalimu, tunawaomba mashabiki wetu wote watakaokuja uwanjani kupaka bleach kwenye ndevu au nywele zao kama ishara ya mshikamano," alisema Kamwe.
Yanga inaingia katika mchezo huo ikiwa na faida ya goli la ugenini, ambapo ushindi wa aina yoyote au sare ya bila kufungana itawavusha kwenda hatua inayofuata.