Yanga SC imeweka wazi kwamba msimu huu haitaki kwenda kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika kwa ajili ya kushiriki tu, bali inataka kupigania taji.
Kocha Mkuu wa Yanga, Manqoba Mngqithi, ameweka wazi malengo yake akisisitiza kuwa kiu yake kubwa ni kuiongoza timu hiyo kutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAFCL).
Akizungumza nchini Botswana wakati kikosi chake kikijiandaa kukabiliana na Gaborone United, katika mchezo ambao baadaye ulimalizika kwa sare ya bao 1-1, Manqoba alisema anaamini Yanga ina uwezo wa kwenda mbali na hatimaye kutwaa ubingwa wa Afrika.
“Lengo langu mimi ni kuwa bingwa Afrika, tutajaribu kufanya hivyo. Naamini tunayo timu inayoweza kushindana na kuwa bingwa wa Afrika,” alisema Manqoba.
Kauli ya Manqoba inaonyesha wazi kuwa benchi la ufundi la Yanga limeweka malengo makubwa zaidi ya yale yaliyowekwa na uongozi wa klabu.
Kwa msimu huu, uongozi wa Yanga umeweka lengo la angalau kufika hatua ya robo fainali, baada ya Wananchi kufanikiwa kucheza hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa misimu mitatu mfululizo.
Lakini Manqoba na benchi lake la ufundi wanaonekana kutamani kuvuka malengo hayo yaliyowekwa na kufika mbali zaidi.
Benchi la ufundi linaamini kikosi walichonacho kina ubora, uzoefu na uwezo wa kushindana na vigogo wa Afrika na kwenda hatua ya juu zaidi.
Juzi Yanga ilishindwa kupata ushindi nchini Botswana baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Gaborone United.
Matokeo hayo yameifanya Yanga kuwa na kazi ya kufanya kwenye mchezo wa marudiano.
Ili kuweka hai ndoto ya Manqoba ya kuwa bingwa wa Afrika, Wananchi sasa wanahitaji kushinda mchezo wa marudiano dhidi ya Gaborone United ili kusonga mbele katika hatua inayofuata kuelekea kwenye raundi ya kwanza na hatimaye kuisaka nafasi ya kucheza hatua ya makundi.