Mshambuliaji wa Yanga, Suleiman Mwalimu, amejibu kwa vitendo na maneno baada ya kuibuka shujaa wa timu hiyo katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Gaborone United ya Botswana.
Mwalimu, ambaye alijiunga na Yanga akitokea Wydad CA baada ya kuikacha Simba katika dirisha hili la usajili, jana aliwapa furaha kubwa mashabiki wa Wananchi baada ya kufunga bao la kusawazisha katika dakika za lala salama na kuifanya Yanga kutoka na sare ya 1-1 ugenini.
Bao hilo lilizua shangwe kubwa kwa mashabiki wa Yanga waliokuwa wamefurika Makao Makuu ya klabu hiyo Jangwani, jijini Dar es Salaam, wakifuatilia mchezo huo.
Lakini zaidi ya bao hilo, Mwalimu alituma ujumbe mwingine muhimu baada ya mchezo huo.
Akizungumza baada ya kuisaidia Yanga kuondoka na matokeo mazuri Botswana, mshambuliaji huyo alisema wazi kuwa anawapenda sana Wananchi na ana furaha kuwa sehemu ya mabingwa hao wa nchi.
Kauli hiyo inakuja ikiwa tofauti na kile ambacho kiungo wa Simba, Clatous Chama ‘Mwamba wa Lusaka’, aliwahi kusema kuhusu hali ya Mwalimu baada ya kuhamia Yanga.
Chama alisema nini?
Chama alipokuwa akisimulia uzoefu wake wa kuondoka Simba na kujiunga na Yanga msimu wa 2024/25, alifichua kuwa yeye binafsi hakufurahia uamuzi huo na hata alijaribu kurejea Simba baada ya kusaini mkataba wa Yanga.
Katika mahojiano yake, Chama alimtaja pia Mwalimu na kudai kuwa mshambuliaji huyo hana furaha baada ya kujiunga na Yanga.
Kauli hiyo iliibua maswali kuhusu hali halisi ya Mwalimu ndani ya Yanga, hasa kwa kuwa uhamisho wake kutoka Simba kwenda Yanga ulikuwa miongoni mwa matukio yaliyofuatiliwa kwa karibu katika dirisha hili.
Lakini jana Mwalimu alionekana kutoa jibu lake mwenyewe.
