Yanga imepata matokeo muhimu ugenini ikiilazimisha Gaborone United sare ya bao 1-1 katika mchezo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika.
Alikuwa ni Seleman Mwalimu 'Gomez' aliyefunga bao muhimu ugenini dakika za jiooooni akimalizia pasi ya kisigino kutoka kwa Mudathir Yahya.
Yanga ilitawala mchezo huo kwa muda mwingi huku Gaborone United wakicheza kwa kujihami zaidi 'walipaki basi'.
Gaborone walifunga bao lao kwenye kipindi cha kwanza kupitia mpira wa adhabu nje kidogo ya 18 likifungwa na Obry Amseb.
Kwa ujumla zilikuwa dakika 90 zilizotawaliwa na Yanga pengine changamoto kubwa ilikuwa kuvunja ukuta wa Gaborone ambao walijilinda na wachezaji 10.
Hata hivyo dakika za lala salama walipoteza umakini pasi mpenyezo kutoka kwa Maxi Nzengeli ikutua mguuni kwa Mudathir aliyetoa pasi ya kisigino kwa Mwalimu.
Yanga sasa ina dakika 90 nyumbani kusaka matokeo muhimu ili kufuzu raundi ya kwanza ikiwa na faida ya bao la ugenini.