Klabu ya Gaborone United imeonekana kutofurahishwa na uamuzi wa Yanga kukataa kutumia basi walilowaandalia kwa ajili ya usafiri wao nchini Botswana.
Gaborone United, ambao ni wapinzani wa Yanga SC katika mchezo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika (CAFCL) ambao utapigwa leo uwanja wa Taifa wa Botswana, walifanya maandalizi mbalimbali kwa ajili ya kuwapokea wageni wao, ikiwemo kuwaandalia basi maalumu la usafiri.
Hata hivyo, Yanga waliamua kutumia usafiri waliouandaa wenyewe, jambo lililoibua malalamiko kutoka kwa wenyeji hao.
Msemaji wa klabu ya Gaborone United amedai walifanya maandalizi hayo kwa gharama kubwa wakitarajia Yanga watatumia huduma hizo kama ilivyokuwa imepangwa.
Kamwe awajibu
Akizungumzia suala hilo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga SC, Ali Kamwe amesema kuwa suala hilo si jambo kubwa na kwamba halikustahili kugeuka kuwa malalamiko.
Kamwe amebainisha kuwa kanuni za mashindano zinamtaka mwenyeji kuhakikisha anaandaa mazingira mazuri kwa ajili ya timu mgeni, lakini hakuna kanuni inayomlazimisha mgeni kutumia usafiri ambao umeandaliwa na wenyeji.
Kamwe alitoa mfano kwamba hata timu zinapokuja Tanzania, baadhi yao huamua kutotumia magari au usafiri wanaoandaliwa na wenyeji kwa sababu mbalimbali.
“Kanuni inamtaka mwenyeji kuandaa mazingira kwa ajili ya mgeni, lakini hakuna kanuni inayomtaka mgeni kutumia alichoandaliwa,” alisema
Yanga pia wamekwenda na chakula na maji yao
Mbali na suala la usafiri, Yanga pia wamefanya maandalizi yao binafsi kuhusu mahitaji mengine wakiwa Botswana.
Kamwe ameeleza kuwa baadhi ya timu zinapokuwa safarini kwa ajili ya mashindano ya kimataifa husafiri na chakula pamoja na maji yao ili kuhakikisha wachezaji wanapata huduma wanazoziamini na walizozoea.
Yanga nao wamefanya hivyo nchini Botswana, ikiwa ni sehemu ya maandalizi yao kwa ajili ya mchezo huo.