Kikosi cha Yanga leo kitashuka uwanja wa Benjamin Mkapa kuikabili Azam Fc ukiwa ni mchezo wa ligi kuu ya NBC
Wananchi wenyewe wanasema kukaa bila kuishuhudia Yanga unaweza kuugua! Zimepita siku 11 tangu walipocheza dhidi ya KMC na kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 mkoani Ruvuma
Leo wataishuhudia timu yao katika mchezo dhidi ya Azam Fc, pale dimba la Mkapa kuanzia saa moja usiku
Ni mchezo ambao utakuwa na ushindani mkali kutokana na historia ya timu hizi kila zinapokutana
Mpaka sasa hakuna timu iliyoshinda mechi nyingi zaidi ya mwenzake na kwa wastani, kila msimu zimekuwa zikigawana matokeo
Msimu uliopita Yanga ilishinda mchezo wa duru ya kwanza na Azam Fc wakashinda mchezo wa duru ya pili
Hata hivyo huu ni msimu mwingine, Yanga imebadilika lakini hata Azam Fc wamebadilika pia
Wananchi wanasaka ubingwa wa 28 wa ligi kuu baada ya kuukosa kwa misimu minne mfululizo, wamedhamiria kutimiza kusudio hilo
Ili kuwa bingwa unapaswa kukusanya alama nyingi kuliko wengine wote na muhimu unapaswa kupata alama nyingi dhidi ya wapinzani wako katika mbio za ubingwa
Hivyo ni mchezo ambao Yanga inahitaji kuondoka na alama zote tatu pamoja na kuwa hautakuwa mchezo mwepesi
Kocha Msaidizi wa Yanga Cedric Kaze amesema wachezaji wako tayari na wanajua aina ya mchezo wanakwenda kucheza dhidi ya Azam Fc
Hii ni siku ya burudani kwa mashabiki wa Yanga kwani kabla ya mchezo watapata burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali
Hivyo kwa mashabiki ni vyema wakawahi mapema uwanjani kwani kuna mambo mengi yameandaliwa kwa ajili yao