Mwenyekiti wa Kamati ya mashindano ya Simba, Swedi Mkwabi amewaita mashabiki wa Simba kuujaza uwanja wa Uhuru siku ya jumapili Septemba 13, 2026 itakapocheza mchezo wa marudiano dhidi ya Mighty Wanderes CAFCL.
Akizungumza muda mfupi baada ya kikosi cha Simba kurejea jijini Dar es salaam wakitokea Malawi, Mkwabi amesema ushindi waliopata ugenini ni matokeo muhimu ambayo yanawaweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele.
Hata hivyo jukumu la kila Mwana Simba ni kuhakikisha wanatimiza malengo yao kwenye mchezo wa marudiano uwanja wa Uhuru.
"Ulikuwa mchezo mgumu lakini ushindi yalikuwa matokeo muhimu sana kwetu. Tumerejea nyumbani, tutajiandaa vyema kwa ajili ya mchezo wa marudiano"
"Tunawaomba mashabiki wetu waje kwa wingi uwanja wa Uhuru siku ya Jumapili ili kuhakikisha tunakwenda kutimiza malengo yetu pamoja," alisema Mkwabi.
Aidha baada ya Simba kucheza hatua ya robo fainali mara kadhaa, Mkwabi amesema msimu huu wanataka kuvuka hatua hiyo wakiweka malengo ya chini ya nusu fainali.
"Wakati huu tumejipanga, tunataka kufika mbali zaidi, nusu fainali na hata fainali," aliongeza Mkwabi.
Baada ya kurejea jijini Dar es salaam leo, uongozi wa Simba uliwapa wachezaji mapumziko ya siku moja ambapo kesho wataanza maandalizi kuelekea mchezo huo ambao Mnyama anahitaji ushindi au matokeo ya sare kutinga raundi ya kwanza