Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi klabu ya Simba Crescentius Magori amesema ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mighty Wonderers katika mchezo wa kwanza wa hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika ni hatua nzuri lakini badi wanapaswa kumaliza kazi kwenye mchezo wa marudiano.
Akizungumza muda mfupi baada ya kikosi cha Simba kurejea jijini Dar es salaam wakitokea Malawi, Magori aliwataka mashabiki kujitokeza kwa wingi uwanja wa Uhuru siku ya Jumapili ili kuhakikisha wanamaliza kazi iliyobaki pamoja.
"Mchezo ulikuwa mgumu, Mighty Wonderers ni timu nzuri tunafurahi tumewezakupata ushindi ugenini lakini kazi bado hatujaimaliza"
"Tunawaomba mashabiki wetu waje kwa wingi uwanja wa Uhuru siku ya Jumapili ili tukamilishe mpango wetu wa kufuzu hatua inayofuata," alisema Magori.
Simba itakuwa na siku 6 za kukamilisha maandalizi yake kuelekea mchezo huo wa mkondo wa pili utakaopigwa Septemba 13 uwanja wa Uhuru, saa 10 jioni.