Kiungo mshambuliaji wa Simba SC, Libasse Gueye, amewapa mzuka wachezaji wenzake kuelekea mchezo wao wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Mighty Wanderers ya Malawi, licha ya yeye kukosekana kwenye mchezo huo utakaopigwa leo Jumapili saa 10:00 jioni.
Gueye amesema mwenendo mzuri wa Simba katika Ligi Kuu Bara, ikiwemo ushindi wa michezo mitano mfululizo, umeongeza nguvu, morali na kujiamini kwa kikosi hicho kuelekea kuanza kwa safari yao ya kimataifa.
Gueye amesema matokeo hayo mazuri yamekuwa sehemu muhimu ya maandalizi ya Simba kabla ya kukutana na Mighty Wanderers, huku akiamini wachezaji wenzake wana uwezo wa kuendeleza kasi hiyo kwenye michuano ya kimataifa.
“Ushindi wa michezo mitano mfululizo umetupa nguvu na kujiamini zaidi. Tunaingia kwenye mchezo huu tukiwa na morali kubwa na tukiwa tayari kupambana,” Gueye amesisitiza.
Gueye hatakuwa sehemu ya kikosi cha Simba leo kutokana na kutumikia adhabu ya kadi nyekundu aliyopata msimu uliopita katika mchezo wa hatua ya makundi dhidi ya Petro Atletico ya Angola.
Kutokuwepo kwake ni pigo kwa upande wa Simba, lakini kauli yake imeongeza hamasa ndani ya kikosi huku akiwataka wachezaji wenzake kutumia nafasi hiyo kuonyesha ubora wao kwenye jukwaa la Kimataifa.