Simba Sc leo inashuka kwenye Uwanja wa Bingu jijini Lilongwe kuvaana na wenyeji wao Mighty Wonderers, katika mchezo wa kwanza wa raundi ya awali ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika (CAFCL).
Mchezo huo unaotarajiwa kuanza saa 10:00 jioni kwa saa za Afrika Mashariki, unatajwa kuwa mtihani mzito kwa wenyeji wanaokabiliwa na rekodi bora ya kimataifa ya Simba SC katika miaka ya hivi karibuni.
Kocha Mkuu wa Simba SC, Steve Barker, ameweka wazi kuwa timu yake haikuja Malawi kutafuta sare, bali kupambana kupata ushindi utakaowarahisishia kazi katika mchezo wa marudiano utakaopigwa jijini Dar es Salaam.
Simba imeingia vitani ikiwa na morali kubwa baada ya kushinda mechi zake tano zilizopita za mashindano ya ndani.
Mighty Wanderers wao wanatarajiwa kutumia faida ya uwanja wa nyumbani na mashabiki wao kujaribu kupata matokeo chanya.
Timu hiyo inapitia kipindi cha mpito kwenye benchi lao la ufundi na matokeo yanayosuasua kwenye ligi ya ndani, ni wazi leo watakuwa na kazi kubwa mbele ya Wekundu wa Msimbazi.
Mchezo huu utachezwa chini ya mwamuzi wa kimataifa Charles Bulu kutoka nchini Ghana, na utarushwa mubashara kupitia chaneli ya Azam Sports 2 HD.