Kocha Mkuu wa Simba Steve Barker amesema kikosi chake kiko Malawi kikiwa na dhamira moja tu, kuonyesha soka safi na kupata ushindi kwenye mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Mighty Wonderers.
Akizungumza kwenye mkutano na wanahabari kuelekea mchezo huo wa hatua ya awali utakaopigwa kesho Jumapili kwenye uwanja wa Bingu, Barker amesema anatambua wanakutana na timu nzuri ambayo ina wachezaji wenye uzoefu ambao pia wako kwenye timu mbalimbali za Taifa.
Hata hivyo amesisitiza kikosi chake kiko tayari kwa mchezo huo na wanalenga kupata matokeo mazuri ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele raundi inayofuata.
"Kila timu iliyoko kwenye michuano hii inataka kuvuka na kusonga mbele kama ilivyo kwetu Simba."
"Mighty Wonderers ni timu nzuri inayoundwa na wachezaji wengi wenye uzoefu na wako katika timu zao za Taifa."
"Lakini sisi tuko hapa kwa ajili ya kuonyesha soka safi na kupata matokeo chanya," alisema Barker.
Kikosi cha Simba kiliwasili Malawi mapema jana ambapo jioni walipata nafasi ya kufanya mazoezi ya kwanza nchini humo.
Leo Simba itakamilisha maandalizi yake ya mwisho kwenye uwanja wa Bingu.